JE, UNAJUA ile hadithi kuhusu Adamu na Hawa na bustani ya Edeni? Watu wengi ulimwenguni wanaijua. Tunakutia moyo uisome hadithi hiyo. U...
JE, UNAJUA ile hadithi kuhusu Adamu
na Hawa na bustani ya Edeni? Watu wengi ulimwenguni wanaijua. Tunakutia
moyo uisome hadithi hiyo. Utaipata katika andiko la Mwanzo 1:26–3:24. Huu ndio muhtasari wa hadithi hiyo:
Yehova Mungu*
anamuumba mwanadamu kutokana na mavumbi na kumwita Adamu, kisha
anamweka katika bustani iliyo katika eneo linaloitwa Edeni. Mungu
mwenyewe ndiye mpandaji wa bustani hii. Imetunzwa vizuri, na ina miti
mingi yenye kupendeza inayozaa matunda. Katikati ya bustani hii kuna
“mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Mungu anawakataza wanadamu wasile
matunda ya mti huo, akisema kuwa wasipotii watapatwa na kifo. Baada ya
muda, Yehova anamuumba Hawa, msaidizi wa Adamu, kutokana na ubavu mmoja
wa Adamu. Mungu anawapa kazi ya kutunza butani na kuwaambia wazaane na
kuijaza dunia.
Hawa anapokuwa peke yake, nyoka
anaongea naye, akimshawishi ale matunda aliyokatazwa akidai kuwa Mungu
amemdanganya na anamnyima kitu fulani kizuri, kitakachomfanya awe kama
Mungu. Anashawishika na kula matunda ya mti huo. Baadaye, Adamu
anajiunga naye kutomtii Mungu. Yehova anachukua hatua na kutangaza
hukumu juu ya Adamu, Hawa, na nyoka. Baada ya wanadamu kufukuzwa kutoka
katika bustani hiyo ya kiparadiso, malaika wanailinda njia ya kuingia
humo.
Wakati fulani lilikuwa jambo la
kawaida kwa wasomi, watu wenye akili, na wanahistoria kukubali kuwa
matukio katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo ni ya kweli na yalitukia.
Siku hizi, watu wengi wanatilia shaka mambo hayo. Lakini wana sababu
gani za kutilia shaka simulizi la Mwanzo kuhusu Adamu, Hawa, na bustani
ya Edeni? Acheni tuchunguze sababu nne kuu.
1. Je, bustani ya Edeni ilikuwa mahali halisi?
Kwa nini watu wana shaka kuhusu jambo
hilo? Huenda falsafa ilichangia kuwapo kwa shaka hizo. Kwa karne
nyingi, wanatheolojia walikuwa wakifikiria kuwa bustani ya Mungu bado
ilikuwa mahali fulani. Hata hivyo, kanisa liliathiriwa na wanafalsafa
Wagiriki kama Plato na Aristotle, walioamini kuwa hakuna kitu kikamilifu
duniani. Ukamilifu ungeweza kupatikana mbinguni pekee. Kwa hiyo,
wanatheolojia wakakata kauli kuwa lazima Paradiso ya kwanza iwe ilikuwa
karibu na mbinguni.*
Wengine walisema kuwa bustani hiyo ilikuwa juu ya mlima mrefu sana hivi
kwamba haingeweza kuathiriwa na dunia iliyopotoka; wengine walisema
ilikuwa katika Ncha ya Kaskazini au Ncha ya Kusini; nao wengine walisema
ilikuwa karibu na au juu ya mwezi. Haishangazi kuwa simulizi kuhusu
bustani ya Edeni lilianza kuonekana kama jambo la kuwaziwa tu. Wasomi
fulani wa kisasa wanasema kuwa habari kuhusu mahali ambapo Edeni ilikuwa
ni upuuzi mtupu, wakisisitiza kuwa hakujawahi kuwapo na mahali kama
hapo.
Hata hivyo, Biblia haielezi kuhusu bustani ya Edeni kwa njia hiyo. Katika Mwanzo 2:8-14,
tunajifunza mambo kadhaa kuhusu eneo hilo. Bustani hiyo ilikuwa
mashariki ya eneo linaloitwa Edeni. Maji katika bustani hiyo yalitoka
katika mto ambao ulikuwa chanzo cha mito minne. Majina ya mito hiyo yote
minne yanatajwa na pia maelezo mafupi kuhusu mahali ilikoelekea. Wasomi
wengi wametamani sana kujua habari kuhusu eneo la Edeni, hivyo wengi
wao wametumia sehemu hii ya Biblia kujaribu kutafuta eneo hilo la kale
liko mahali gani. Hata hivyo, wasomi hao wametoa maoni mengi
tofauti-tofauti kuhusu eneo hilo. Je, hilo linamaanisha kuwa maelezo
halisi kuhusu eneo la Edeni, bustani hiyo, na mito yake ni uwongo au ni
hadithi tu?
Wazia: Matukio ya simulizi la bustani
ya Edeni yaliyotokea miaka 6,000 hivi iliyopita. Musa ndiye aliyeandika
simulizi hilo, na huenda alitumia masimulizi yaliyopitishwa kwa mdomo
au hata maandishi fulani yaliyokuwapo wakati huo. Hata hivyo, Musa
aliandika simulizi hilo miaka 2,500 hivi baada ya matukio hayo. Tayari
matukio katika Edeni yalikuwa historia ya kale. Je, baada ya karne
nyingi kupita, huenda alama hizo kuu kama mito imebadili mikondo yake?
Uso wa dunia unabadilika kila mara. Eneo ambapo bustani ya Edeni ilikuwa
linaathiriwa sana na matetemeko ya ardhi—asilimia 17 ya matetemeko yote
duniani, yanatukia katika eneo hilo. Katika maeneo kama hayo,
mabadiliko katika uso wa dunia ni jambo la kawaida. Zaidi ya hayo,
huenda Gharika ya siku za Noa ilibadili uso wa eneo hilo katika njia
ambazo hatuwezi kuzielewa leo.*
Hata hivyo, kuna mambo machache ya
hakika tunayojua: Simulizi la kitabu cha Mwanzo linataja kuwa bustani ya
Edeni ilikuwa mahali halisi. Mito miwili kati ya mito minne inayotajwa
katika simulizi hilo—Efrati na Tigri, au Hidekeli—bado ipo hadi leo, na
baadhi ya vyanzo vyake viko karibu-karibu. Simulizi hilo linataja majina
ya maeneo ambapo mito hiyo ilipitia na hata inataja kihususa maliasili
zinazojulikana sana katika eneo hilo. Habari hizo ziliwasaidia Waisraeli
wa kale waliosoma simulizi hilo kuelewa mambo mengi.
Je, hadithi na hekaya zinawasaidia
watu kuelewa mambo vizuri? Au huwa zinakosa mambo hususa ambayo yanaweza
kuthibitishwa kwa urahisi kuwa ya kweli au ya uwongo, au hata
kukanushwa? Hadithi nyingi huanza hivi: “Hapo zamani za kale katika nchi
moja ya mbali.” Lakini, historia hutoa habari hususa, kama lifanyavyo
simulizi kuhusu Edeni.
2. Je, tunaweza kuamini kuwa Mungu alimuumba Adamu kutokana na mavumbi na Hawa kutokana na ubavu mmoja wa Adamu?
Wanasayansi wa kisasa
wamethibitisha kuwa mwili wa mwanadamu una elementi fulani—kama vile
hidrojeni, oksijeni, na kaboni—ambazo zinapatikana katika udongo. Lakini
elementi hizo zilikusanywa kwa njia gani na kuwa mwili wa kiumbe hai?
Wanasayansi wengi wanataja kuwa
uhai ulijitokeza wenyewe, ukianzia na viumbe visivyo tata na kubadilika
polepole, na baada ya mamilioni ya miaka ukawa tata hata zaidi. Hata
hivyo, maneno “visivyo tata” yanaweza kupotosha kwa kuwa viumbe vyote
vilivyo hai—hata chembe ndogo zisizoweza kuonekana kwa macho—ni tata
sana. Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kuwa kuna aina yoyote ya
uhai uliojitokeza wenyewe au unaoweza kujitokeza wenyewe. Badala yake,
kuna uthibitisho ulio wazi kuwa viumbe vyote vilibuniwa na mbuni mwenye
akili nyingi zaidi kuliko ya wanadamu.*—Waroma 1:20.
Hebu wazia ukisikiliza muziki mtamu
au ukifurahia kuona mchoro wenye kupendeza au ukistaajabia jambo fulani
la kitekinolojia, kisha unasisitiza kuwa hakuna mtu aliyebuni vitu
hivyo. Bila shaka, hilo ni jambo lisilopatana na akili! Lakini vitu
hivyo haviwezi kufikia utata, uzuri, au hata hekima iliyohusika katika
kuubuni mwili wa mwanadamu. Ni jambo lisilowazika kusema kuwa mwili wa
mwanadamu haukuumbwa. Zaidi ya hayo, simulizi la Mwanzo linaeleza kuwa
kati ya viumbe vyote duniani, wanadamu peke yao ndio walioumbwa kwa
mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26)
Ndiyo maana ni wanadamu pekee walio na uwezo wa kubuni vitu kama
afanyavyo Mungu, wakati fulani wakibuni vitu vyenye kupendeza kama
muziki, sanaa, na tekinolojia. Hivyo, si ajabu kwamba Mungu ana uwezo
mkubwa wa kubuni kuliko ule tulio nao.
Je, kuna ugumu wowote kumuumba mwanamke kwa kutumia ubavu wa mwanamume?*
Mungu angeweza kutumia njia nyingine, lakini mbinu hii aliyotumia
kumuumba mwanamke ina umaana mkubwa. Alitaka mwanamume na mwanamke wawe
na uhusiano wa karibu, kana kwamba wao ni “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24)
Jinsi mwanamume na mwanamke wanavyokamilishana, wakifanyiza uhusiano
thabiti ambao unawaimarisha wote wawili, ni uthibitisho ulio wazi kuwa
kuna Muumba mwenye hekima na upendo.
Zaidi ya hayo, wataalamu wa kisasa
wa chembe za urithi wamekiri kuwa yaelekea wanadamu walitokana na
mwanamume na mwanamke mmoja. Kwa hiyo, je, simulizi la Mwanzo ni la
kweli?
3. Je, habari kuhusu mti wa ujuzi na mti wa uzima ni hadithi tu?
Kwa kweli, simulizi la Mwanzo
halionyeshi kwamba miti hiyo ilikuwa na nguvu fulani zisizo za kawaida.
Badala yake, ilikuwa miti halisi ambayo Yehova aliiweka iwakilishe jambo
fulani.
Je, wanadamu hawafanyi hivyo
nyakati nyingine? Kwa mfano, hakimu anaweza kumwonya mtu asiidharau
mahakama. Hilo halimaanishi kwamba hakimu anazuia viti, meza, nembo za
taifa, kuta, na vitu vingine vilivyo ndani ya mahakama hiyo
visidharauliwe, bali anataka kulinda mfumo wa kisheria unaowakilishwa na
mahakama hiyo. Watawala mbalimbali wametumia fimbo ya ufalme na taji
kuwa ishara ya mamlaka yao.
Hivyo, ile miti miwili iliwakilisha
nini? Kumekuwa na maoni mengi yasiyoeleweka kuhusu jambo hilo. Kuna
jibu la kweli na rahisi, lakini lenye umaana mkubwa sana. Mti wa ujuzi
wa mema na mabaya unawakilisha pendeleo ambalo ni la Mungu pekee, yaani,
haki ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya. (Yeremia 10:23)
Ndio sababu lilikuwa kosa kuiba matunda ya mti huo! Kwa upande
mwingine, mti wa uzima uliwakilisha zawadi ambayo Mungu pekee ndiye
aliye na uwezo wa kuitoa, yaani, uzima wa milele.—Waroma 6:23.
4. Je, nyoka anayesemwa kuwa aliongea, ni hadithi tu?
Kwa kweli, huenda simulizi hilo la
Mwanzo likawa gumu kueleweka, hasa ikiwa msomaji hatazingatia Biblia
yote nzima. Hata hivyo, pole kwa pole Maandiko hufunua fumbo hilo lenye kutatanisha.
Ni nani au ni nini kilichomwezesha
nyoka kuongea? Watu wa Israeli la kale walijua mambo mengine
yaliyowasaidia kupata uelewevu zaidi kuhusu jinsi nyoka huyo
alivyohusika. Kwa mfano, walijua kwamba ingawa wanyama hawaongei, kiumbe
wa roho anaweza kumfanya mnyama aonekane kama anaongea. Musa pia
aliandika simulizi kuhusu Balaamu. Simulizi hilo linasema kuwa Mungu
alimtuma malaika amfanye punda wa Balaamu aongee kama mwanadamu.—Hesabu 22:26-31; 2 Petro 2:15, 16.
Je, roho wengine, kutia ndani wale
ambao ni maadui wa Mungu, wanaweza kufanya miujiza? Musa alikuwa
amewaona makuhani wa Misri wenye kufanya miujiza wakiiga baadhi ya
miujiza ya Mungu, kama kugeuza fimbo iwe nyoka. Uwezo wa kufanya miujiza
kama hiyo ungeweza tu kutoka kwa maadui wa Mungu walio katika makao ya
roho.—Kutoka 7:8-12.
Pia, yaelekea kuwa Musa ndiye
aliyeongozwa na roho ya Mungu kuandika kitabu cha Ayubu. Kitabu hicho
kinaeleza mambo mengi kumhusu adui mkubwa wa Mungu, Shetani, ambaye kwa
uwongo alitilia shaka utimilifu wa watumishi wa Yehova. (Ayubu 1:6-11; 2:4, 5)
Je, Waisraeli hao wa kale walikata kauli kuwa Shetani alimtumia nyoka
katika bustani ya Edeni, na kumfanya aonekane kama anaongea na hivyo
kumdanganya Hawa avunje utimilifu wake kwa Mungu? Huenda ikawa hivyo.
Je, Shetani ndiye aliyemfanya nyoka aseme uwongo? Baadaye Yesu alimtaja Shetani kuwa ‘mwongo na baba ya uwongo.’ (Yohana 8:44)
“Baba ya uwongo” ndiye aliyesema uwongo wa kwanza kuwahi kusemwa
duniani. Uwongo huo wa kwanza unapatikana katika maneno ambayo nyoka
alimwambia Hawa. Akipinga onyo la Mungu kuwa kula matunda yaliyokatazwa
kutasababisha kifo, nyoka alisema hivi: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4)
Kwa wazi, Yesu alijua kuwa Shetani alimtumia nyoka kusema uwongo.
Ufunuo ambao Yesu alimpa mtume Yohana unadhihirisha jambo hilo, kwa
kumwita Shetani “nyoka wa zamani.”—Ufunuo 1:1; 12:9.
Je, itakuwa kupita mipaka kuamini
kuwa kiumbe wa roho mwenye nguvu aliweza kumtumia nyoka na kumfanya
aonekane kama anaongea? Ingawa wanadamu hawana nguvu kama viumbe wa
roho, wao pia wanaweza kufanya sanamu ionekane kama inatoa sauti, kumbe
ni mwanadamu anayetoa sauti hiyo.
Uthibitisho Ulio Hakika Kabisa
Je, hukubali kuwa watu wanaotilia
shaka simulizi la Mwanzo hawana msingi mzuri wa kufanya hivyo? Kwa
upande mwingine, kuna uthibitisho mwingi wa kwamba simulizi hilo ni
historia ya kweli.
Kwa mfano, Yesu Kristo anaitwa “shahidi mwaminifu na wa kweli.” (Ufunuo 3:14)
Kwa kuwa alikuwa mtu makamilifu, Yesu hakuwahi kusema uwongo wala
kuipotosha kweli. Zaidi ya hayo, alifundisha kuwa alikuwapo muda mrefu
kabla ya kuja duniani akiwa mwanadamu—na hata, alikuwa kando ya Baba
yake, Yehova, “kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:5)
Kwa hiyo, alikuwa hai wakati uhai ulipoanza duniani. Hivyo basi, Yesu
ambaye ndiye shahidi mwenye kutegemeka zaidi ya mashahidi wote anasema
nini?
Yesu aliwataja Adamu na Hawa kuwa
watu halisi. Alitaja ndoa yao alipokuwa akifafanua kanuni ya Yehova
kuhusu kufunga ndoa na mwenzi mmoja tu. (Mathayo 19:3-6)
Ikiwa Adamu na Hawa hawakuwahi kuwapo na bustani walimoishi ilikuwa
hadithi tu, basi ama Yesu alikuwa amedanganywa au alikuwa mwongo. Yesu
hangeweza kudanganywa wala kusema uwongo! Yeye alikuwa mbinguni
akitazama tukio hilo lenye kuhuzunisha lilipotokea
katika bustani ya Edeni. Je, kunaweza kuwa na uthibitisho mwingine wenye
kutegemeka zaidi ya huo?
Kwa hiyo, kutoamini simulizi la
kitabu cha Mwanzo ni kukosa imani katika Yesu. Pia, kutoamini simulizi
hilo kunafanya isiwezekane kuelewa baadhi ya mafundisho muhimu ya Biblia
na ahadi zake zenye kufariji. Acheni tuone kwa nini inaweza kuwa hivyo.