Familia ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), imelitaka Bunge kutoa fedha za matibabu yake kama halitaki mtunga sheria w...

Familia ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), imelitaka Bunge kutoa fedha za matibabu yake kama halitaki mtunga sheria wake huyo akafukuzwe hospitalini alikolazwa.
Lissu amelazwa katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Luvein
nchini Ubelgiji tangu mapema mwezi huu baada ya kutibiwa Hospitali ya
Nairobi nchini Kenya kwa miezi minne.
Msemaji wa familia ya Lissu, wakili Alute Mughwai,
aliwaeleza waandishi wa habari ofisini kwake jana kuwa miezi ni mitano
sasa Lissu hajapata stahiki zake kimatibabu kama Mbunge.
“Tumemaliza miezi mitano tangu kutokea kwa tukio la
kushambuliwa kwa Lissu na Bunge kama taasisi limeshindwa kutoa fedha za
matibabu kwa mwenzao," alisema Mughwai.
“Sasa Lissu atalaumiwaje? Akilia Mungu wangu mbona
umeniacha, Bunge langu mbona limeniacha... au wanataka afukuzwe hapo
hospitalini kwa kukosa fedha za matibabu?
“Mpaka sasa hatujui kinachoendelea. Tunaweza kusema ni
siasa au kwa namna nyingine tunaweza kutafsiri kuwa sababu Lissu ni
mkosoaji mzuri wa serikali bungeni.
“Waheshimiwa hawa wanataka mwenzao kuwa kilema au kupoteza
maisha? Cha msingi wanapaswa kutoa haki za msingi ambazo sisi tumeona
zinacheleweshwa kwa makusudi.”
Bunge lilishasema hata hivyo kwamba Lissu alifuata matibabu
nje ya nchi kinyume na utaratibu wa bima ya afya ya wabunge, hivyo kuwa
kikwazo cha kuhudumiwa kwake.
Lissu (49) alipigwa risasi tano na watu wasiojulikana akiwa
kwenye gari nyumbani kwake Area D mjini Dodoma Septemba 7, mwaka jana.
Jumla ya risasi 32 zilirushwa na watu hao kwa mujibu wa taarifa za
Bunge.
Akizungumzia mawasiliano ya familia na ofisi ya Bunge,
alisema Desemba 15, mwaka jana, alitoa mrejesho kwa vyombo vya habari
kuhusu barua waliyoandikiwa na Katibu wa Bunge ikiwataka familia hiyo
kutoa ufafanuzi wa haki zipi ambazo Lissu anatakiwa kupewa na Bunge.
Alisema waliandika barua ya kuomba ufafanuzi huo, Desemba
13, mwaka jana, na barua hiyo ilipokelewa na Ofisi ya Bunge Desemba 18,
mwaka jana na ilipokelewa kwa njia ya barua za haraka ya DHL.
“Tulichoomba ufafanuzi ni kuhusu fedha za matibabu, stahiki
za usafiri wa kwenda nje ya nchi pamoja na posho ya kujikimu kwa yule
anayemuangalia hospitalini," alisema.
“Bunge ilitoa majibu Desemba 10, mwaka jana, kupitia kwa
Katibu wa Bunge ambapo alidai kuwa barua hiyo iliwaelekeza kurudia
utaratibu wa kufuata utaratibu ambao bunge linatumia kwa ajili ya
matibabu ya wabunge pindi wabunge wanapokwenda kupewa matibabu,”
alisema.
Aidha alisema baada ya kurudia kufanya marekebisho ya barua
hiyo, Katibu wa Bunge aliwajibu Januari 10, mwaka huu, kuwa Wizara ya
Afya imeunda timu ya madaktari bingwa kwenda Nairobi kumuangalia Lissu
wakati wakitambua kuwa mbunge huyo Januari 6, mwaka huu,
alishasafirishwa kwenda nje ya Afrika kwa ajili ya matibabu.
Akizungumzia afya ya Lissu, Mughwai alisema kwa sasa anaendelea vizuri na mazoezi ya viungo, ili kuimarisha afya yake.
Alisema aliwasiliana na Lissu Jumapili ambapo alimweleza anaendelea vizuri na mazoezi akiwa anafanya mara tatu kwa siku.
Alisema mazoezi anayofanyishwa kwa sasa ni kupanda ngazi sita na kuvuta vitu vizito.
Aidha alidai kwa mguu ambao ulipata majeraha makubwa
unaweza kustahimili kusukuma kitu chenye uzito kwa kilo 25 na kwamba
mazoezi yataendelea hadi hapo atakapo kuwa vyema kiafya.



